UAMUZI WA YANGA KUJITOA KOMBE LA MAPINDUZI HAUKUWA WA BUSARA


Klabu ya Yanga ya Dar es Salaam imechukua hatua ya kushangaza ya kujitoa kwenye michuano ya Kombe la Mapinduzi inayoendelea Zanzibar katika dakika za mwisho.

Uongozi wa Yanga ulichukua hatua hiyo siku moja kabla ya mashindano hayo yanayoshirikisha timu 12 kutoka Kenya, Uganda na wenyeji Tanzania kuanza.

Kwa kweli hatua hii ilikuwa ya ghafla mno na tunaamini imewakwaza na kuwapa mtihani  mkubwa waandaaji wa mashindano hayo.

Itiliwe maanani kwamba mashindano hayo ya mwaka huu ni makubwa zaidi na yamepewa uzito mkubwa kwa vile yanafanyika wakati Zanzibar inasherehekea miaka 50 ya Mapinduzi. Kitendo cha Yanga kujiondoa kwenye mashindano hayo tena dakika za mwiso kimeshangaza hasa kwa kuzingatia uhusiano wa klabu ya Yanga na Mapinduzi ya Zanzibar.

Historia inaonyesha kuwa aliyekuwa Rais wa kwanza wa Zanzibar, Abeid Amani  Karume aliwahi kutumia fedha za wananchi wa Zanzibar katika kusaidia kujenga makao makuu ya klabu ya Yanga yaliyopo Jangwani, Dar es Salaam.

Sasa inashangaza kwa uongozi wa Yanga kusahau  historia hiyo na kujitoa katika mashindano yanayotukuza Mapinduzi hayo ya mwaka 1964.

Ukiacha suala hilo la kihistoria, mashindano hayo ya Zanzibar yalikuwa muhimu mno kwa Yanga katika maandalizi yake ya mzunguko wa pili wa Ligi Kuu Bara na michuano ya kimataifa ya Ligi ya Mabingwa Afrika ambayo wanashiriki mwaka huu.

Yanga ingeshiriki  mashindano hayo timu yake ingepata nafasi ya kujua upungufu na udhaifu wake kwani katika hatua za awali ingepambana na Azam ya Dar es Salaam na Tusker ya Kenya ambazo ni timu kubwa na ngumu.

Kuondoa benchi la ufundi na kuitumia kama ndiyo sababu ya kujitoa kwenye mashindano hayo hakutoshi kwani klabu kadhaa zimekuwa zikifukuza makocha lakini zinaendelea na mechi zinazowakabili.

Kama uongozi wa Yanga ungekuwa umejipanga vizuri ungekuwa tayari na kocha mpya ambaye angeitumia michuano ya Kombe la Mapinduzi kuona na kufahamu aina ya wachezaji alionao. Yanga ni lazima ijifahamu kuwa ni klabu kubwa na yenye mashabiki wengi nchini kwa hiyo inatakiwa kutafakari kwa makini kabla ya kuchukua uamuzi wowote ule.

Ni dhahiri kwamba kujitoa kwa Yanga kwenye mashindano hayo kutawaathiri sana waandaaji hasa kwenye mapato kwani mechi za Yanga zilitarajiwa kuwavutia mashabiki wengi.

Lakini, kama Yanga ingejitoa mapema katika mashindano hayo na kuukataa mwaliko wa kushiriki kungewapa nafasi waandaaji kualika timu kubwa kwenye mashindano hayo na ambayo ingepata nafasi ya kujiandaa kabla ya kwenda kwenye mashindano.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments: