WANAFUNZI 300 ELIMU YA JUU KUKOSA MIKOPO


Zaidi ya wanafunzi 300 wa elimu ya juu wa vyuo mbalimbali watakosa mikopo kutoka Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB), kutokana na kushindwa kujaza fomu za kuomba mikopo katika kipindi kilichowekwa. 
Watakaokosa mikopo hiyo kwa mwaka wa masomo wa 2013/2014 ni kuanzia mwaka wa pili na kuendelea, ambao hawakujaza fomu za kuonyesha taarifa zao mpya kwa bodi. 
Wanafunzi hao walitakiwa kuwasilisha maombi ya kupewa mikopo kati ya Mei hadi Julai 30, mwaka huu.
Mkugenzi Msaidizi wa Habari, Elimu na Mawasiliano wa HELSB, Cosmas Mwaisobwa, aliyasema hayo jana jijini Dar es Salaam alipozungumza na waandishi kuhusu utendaji wa kazi wa bodi hiyo. 
Mwaisobwa alisema kwa kuwa wanafunzi hao hawakujaza fomu za kuomba mikopo, mwaka huu hawatapata fursa hiyo na kwamba kwa mujibu wa utaratibu wao, kila mwaka lazima mwanafunzi aombe. 
Alisema wanafunzi watakaokosa fursa hiyo ya mikopo wameanza masomo yao katika vyuo mbalimbali nchini na kwamba  HESLB haijui sababu zilizowafanya wasiombe. 
Kuhusu ufanisi katika utoaji wa mikopo, Mwaisobwa alisema idadi ya wanafunzi wanaoomba mikopo imeongezeka kutoka 42,729 mwaka 2005/2006 hadi kufikia wanafunzi 97,348 mwaka 2012/2013. 
Aidha, Mwaisobwa alisema bajeti ya kuwakopesha wanafunzi imeongezeka kutoka Sh. bilioni 56.1 mwaka 2005/2006 hadi kufikia Sh. bilioni 306 mwaka 20012/2013. 
Alisema mwaka huu serikali imeitengea bodi hiyo Sh. bilioni 325 kwa ajili ya kuwakopesha wanafunzi wapya, 31,647 na 62,376 wanaondelea na masomo yao katika vyuo mbalimbali. 
Wakati wanafunzi hao wakikosa fursa ya mikopo, mapema mwezi huu, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa, aliitaka bodi hiyo kuendelea kutoa huduma kwa ufanisi na weledi mkubwa kwa mwaka huu wa masomo ili kuepusha migogoro ya wanafunzi kuhusu mikopo.
CHANZO: NIPASHE
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments: