KASEJA AMHENYESHA DIDA YANGA


UMAHIRI wa kipa, Juma Kaseja na Ally Mustapha ‘Barthez’, umemhenyesha Deo Munishi ‘Dida’ ambaye analazimika kukesha mazoezini ili asichuje.

Dida ametamka kuwa ubora wa makipa hao unamfanya afanye kazi ya ziada ambayo anahisi hakuwahi kuifanya katika klabu nyingine zote alizowahi kucheza, pia anaogopa kupigwa benchi na Kaseja kama enzi hizo walipokuwa Simba pamoja.

Kiwango cha Dida kimeimarika kwa sasa na mwenyewe anasema: “Ubora wangu umeongezeka na kuwa juu kwa sababu ya uwepo wa Kaseja na Barthez, ni makipa mahiri kwenye ligi.

“Kwa sababu ya ubora wao, inanifanya nisibweteke, nijitume ili niwe bora zaidi na zaidi. Kama nitabweteka na kuwa chini ya kiwango hata kidogo tu, ni wazi sitapata namba.

“Lakini kama ningekua nacheza kikosi kimoja na makipa wengine wasio na uwezo, lazima ningebweteka kwa sababu ningekosa ushindani na kiwango kingebaki kama kilivyo kwa kukosa changamoto.”

Dida anatarajia kuanza mazoezi mwishoni mwa wiki hii, alikuwa kwenye mapumziko akiuguza kidonda kwenye bega la kushoto.

Alijikata na geti nyumbani kwake, lakini aliibua tatizo lingine baada ya kupakaa dawa ya spiriti nyingi iliyomuunguza na kusababisha kidonda hicho kuongezeka. Yeye amesisitiza anaendelea vizuri na atarudi uwanjani akiwa na kasi hiyo hiyo.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments: