HUU NDIO UJUMBE WA LOWASSA KWA WANASIASA WASIOMPENDA....

WAZIRI Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, amesema yuko imara na hakatishwi tamaa na maneno ya baadhi ya wanasiasa dhidi ya harakati zake za kisiasa.

Lowassa ametoa kauli hiyo mwishoni mwa wiki iliyopita, wakati akizungumza katika harambee ya ujenzi wa Shule ya Msingi ya Kanisa la African Inland Church of Tanzania (AICT) mjini Kahama, Mkoa wa Shinyanga.

Alisema, wanasiasa wanaomshambulia na kueneza mabaya dhidi yake hawambabaishi.

“Si nia yangu kuwajibu hao wanaonisema sema..mimi niko imara kama ilivyo kuwa jana, juzi..na nitaendelea kuwa imara kwani naamini anayenilinda bado yuko na mimi. Nayaweza haya yote kwa yeye anitiaye nguvu,” alisema Lowassa.

Lowassa alirejea kauli yake ambayo alikwishaitoa hadharani mara kadhaa, kuwa yeye siyo tajiri wa fedha bali wa watu na kuwashangaa wale ambao wamekuwa wakihangaika kuwajua marafiki zake wanaomsindikiza katika harambee za kuchangia shughuli za kimaendeleo anazozifanya katika sehemu mbalimbali nchini.

Kabla ya Lowassa kuzungumza katika hafla hiyo, Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Shinyanga, Hamis Mgeja, alisema kuwa kuna kikundi cha wanasiasa wahuni wanaojaribu kumkatisha tamaa Lowassa kwa maneno machafu dhidi yake.

“Kuna kikundi cha wanasiasa wahuni, wenye wivu na roho ya korosho dhidi ya Lowassa, wanasema sema maneno ya hovyo hovyo ya kihuni, lakini sisi tunasema usikate tamaa huo ni wivu tu, kazi unazozifanya kulitumikia taifa hili kila mtu anaziona,” alisema Mgeja.

Kauli hiyo ya Mgeja inafuatia kauli zenye mwelekeo wa shutuma ambazo amekuwa akielekezewa Lowassa na baadhi ya wanasiasa, kuwa anatumia fedha chafu kuchangia shughuli za maendeleo ya kijamii.

-Mtanzania
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments: