JESHI LA POLISI LATANGAZA DAU LA MILIONI 100 KWA MTU YEYOTE ATAKAYELITAJA KUNDI LINALOMWAGIA WATU TINDIKALI


Jeshi la Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, limetangaza dau la Sh100 milioni kwa mtu atakayewezesha kupatikana kwa taarifa za kundi la uhalifu linalojihusisha na vitendo vya kuwamwagia maji baadhi ya watu yanayodhaniwa ni tindikali. 


Hatua hiyo inatokana na vitendo hivyo kushamiri maeneo mbalimbali nchini.
 

Kamanda wa Polisi Kanda hiyo, Suleiman Kova, alisema vitendo hivyo havipaswi kuvumiliwa na kuwaomba wananchi kutoa ushirikiano kwa kuwafichua watu hao.

“Nimeamua kuomba fedha hizi serikalini ili nimpe mtu atakayewezesha kupatikana kwa taarifa hizo, hatimaye kukomesha vitendo hivi. Kemikali hii imekuwa na madhara makubwa,” alisema Kova.

 

Hivi karibuni Mkurungezi wa Maduka ya Home Shopping Center, Mfanyabiashara wa Lebonon na raia wawili wa Uingereza walimwagiwa maji yanayodhaniwa ni tindikali.

 

Wakati huohuo, polisi linamshikilia raia wa Uingereza kwa tuhuma za kukutwa na nyara mbalimbali za Serikali zenye thamani ya zaidi ya Sh100 milioni, vikiwamo vipande vinane vya meno ya tembo.

Kova alisema mtuhumiwa huyo ambaye ni Mkurugenzi wa Kampuni ya Usafirishaji Mizigo (TALL), alikamatwa juzi saa 2:00 usiku maeneo ya Mbezi Beach, wilayani Kinondoni.

Alisema alipopekuliwa nyumbani kwake alikutwa na meno 20 na kucha 22 za Simba, shanga mbalimbali zilizotengenezwa kwa meno ya tembo, Kasuku na nyara nyingine ambazo hairuhusiwi kumiliki bila kibali.
 

Alisema uzito wa nyara hizo ni kilo 25, walimkuta na mawe mbalimbali yanayodhaniwa ni madini sambamba na ganda moja la bomu lenye ukubwa mita 130.
TOA MAONI YAKO HAPA CHINI

0 comments: